MKOA wa Kilimanjaro umeongoza katika matokeo ya mtihani wa darasa la saba kwa kufaulisha kwa asilimia 62.41 na kuibuka wa kwanza huku mkoa wa Morogoro ukishika mkia kwa kupata asilimia 29.83.
Waziri wa Elimu na Utamanduni, Bw. Joseph Mungai, alitangaza matokeo hayo jana kwa waandhisi wa habari na viongozi mbali mbali katika ukumbi wa mikutano wa Mkuu wa Mkoa wa Iringa.
Waziri Mungai alisema jumla ya wanafunzi 493,946 walifanya mtihani wa darasa la saba Septemba mwaka huu, ambapo wanafunzi 305,062 sawa na asilimia 61.76 walifaulu mtihani huo.
Alisema wasichana 131,312 walifanya vizuri katika mtihani huo ambapo kufaulu kwao ni sawa na asilimia 54.58 huku wavulana 173,750 sawa na asilimia 68.58 ndio waliofaulu.
Akifafanua matokeo hayo kwa kila mkoa na asilimia ilizopata kwenye mabano, Waziri Mungai alitaja mikoa kama ifuatavyo: Kilimanjaro (62.41%), Mara (56.05%), Dar es Salaam (54.8%), Mbeya (53.37%), Arusha (47.98%), Iringa (47.87%) na Manyara (45.54%)
Mingine ni Ruvuma (43.15%), Kagera(41.58%), Kigoma (41.34%), Mtwara (40.42%), Dodoma (39.77%), Shinyanga (39.36%), Mwanza (39.32%), Lindi (36.73%), Pwani (35.91%), Rukwa (35.82%), Tanga (34.26%), Singida (31.11), Tabora (30.15) na Morogoro (29.83).
Waziri Mungai aliipongeza mikoa ya Kilimanjaro, Mara, Dar es Salaam, Mbeya na Arusha, kwa kuongoza katika mitihani hiyo.
Hata hivyo alisema matokeo kwa waliofaulu mwaka huu ni bora zaidi katika mikoa 20 ikilinganishwa na mwaka jana lakini mkoa wa Mbeya pekee ndio ulioshindwa kuboresha matokeo hayo mwaka huu.
Pia Waziri Mungai alizitaja halmashauri za manispaa na miji ambazo zimefanya vyema katika mtihani huo kwa kutinga nafasi ya tano bora kuwa ni Mbeya Mjini ambayo alipata asilimia 91.3, Moshi Manispaa (87.7%), Iringa Mjini (82.8%), Kigoma Mjini (79% ) na Mwanza Mjini (65.2%).
|